Yaweka historia kuwa jumba la kwanza la sanaa kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya Art OnO nchini Korea Kusini
Kati ya tarehe 2 hadi 5 Aprili, jambo la kipekee lilitokea jijini Seoul, Korea Kusini. Ndani ya kituo kikubwa cha maonesho katikati ya jiji hilo, jumba la sanaa kutoka Dar es Salaam lilisimama bega kwa bega na taasisi mashuhuri za sanaa kutoka duniani kote.

Rangi Gallery, iliyoanzishwa na kuendeshwa na mwanasheria aliyebadili taaluma na kuwa msimamizi wa sanaa, Lorna Mashiba Albou, imeweka historia kwa kuwa jumba la kwanza kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya Art OnO, moja ya maonesho ya sanaa yenye upekee mkubwa barani Asia. Hii ni hatua ya kihistoria kwa Tanzania na ishara ya kuendelea kufunguka kwa sanaa ya nchi kimataifa.
Maonesho ya Art OnO, yenye maana ya Art One and Only, yaliyofanya toleo lake la tatu na kufanyika katika kituo cha maonesho cha SETEC jijini Seoul. Mwaka huu, yaliwakutanisha majumba 35 ya sanaa na taasisi kutoka nchi 12, zikiwemo Japan, Ujerumani na Uswisi. Tofauti yake kuu ni mtazamo wake wa kuleta pamoja majumba ya sanaa ya kibiashara na taasisi zisizo za kibiashara katika jukwaa moja la usawa. Katika mazingira kama haya, kushiriki pekee yake ni uthibitisho wa ubora wa kazi zinazowasilishwa.

Katika maonesho hayo, Rangi Gallery iliwasilisha kazi za wasanii wanne wanawake kutoka Tanzania ambao ni Theresia Venance, Tulsi Patel, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo. Kila mmoja alileta mtazamo wake wa kipekee unaoonesha upeo na hisia za sanaa ya kisasa ya Kitanzania.

Theresia Venance aliwasilisha picha za maumbo ya binadamu zinazoangazia uzoefu wa mwanamke na uimara wake kwa namna ya karibu na yenye kugusa hisia za wengi. Valerie Asiimwe Amani alionesha kazi za mixed media zinazochunguza masuala ya ulimwengu na utambulisho wa kitamaduni kwa utulivu lakini kwa kina. Turakella Editha Gyindo aliwasilisha kazi zinazogusa mila, mabadiliko na uponyaji, huku Tulsi Patel akitumia maji, mtiririko wake na mawimbi yake kama taswira ya kina ya mwili wa binadamu.
Akizungumzia ushiriki huo, Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Rangi Gallery, Lorna Mashiba Albou, alieleza kuwa licha ya wasanii wote waliowasilishwa kuwa wanawake, hilo halikupangwa mahsusi bali lilitokana na ubora wa kazi zao.

“Ukweli ni kwamba wanawake hawa wanne wameiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa hili la kimataifa. Hii pia inaonesha namna vipaji vya wasanii wanawake vinavyoendelea kujitokeza na kutambulika duniani,” alisema.
Ushiriki huu unaashiria mwanzo wa safari pana zaidi kwa sanaa ya Tanzania katika majukwaa ya kimataifa. Wasanii wawili kati ya hao, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo, wanatarajiwa kuiwakilisha Tanzania katika Maonesho ya Venice Biennale 2026, mojawapo ya majukwaa yenye hadhi kubwa zaidi duniani katika sanaa. Aidha, Lorna Mashiba Albou ameteuliwa kuwa msimamizi wa banda la Taifa la Tanzania katika maonesho hayo. Kutoka Seoul hadi Venice, mwelekeo ni sanaa ya kisasa ya Tanzania inaendelea kujijenga kimataifa, na Rangi Gallery iko mstari wa mbele kufungua milango hiyo.

Mbali na mafanikio ya kisanaa, ushiriki huo pia ulikuwa na uzito wa kidiplomasia. Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Bw. Togolani Edriss Mavura, alihudhuria maonesho hayo na kushuhudia kazi zilizooneshwa. Uwepo wake uliashiria kuwa tukio hilo halikuwa la sanaa pekee, bali pia lilikuwa jukwaa muhimu la kubadilishana utamaduni kati ya Tanzania na Korea Kusini.

Rangi Gallery ilianzishwa Dar es Salaam na Mashiba Albou, ambaye alifanya kazi kwa zaidi ya muongo mmoja kama mwanasheria wa kampuni kabla ya kuhamia katika uchumi wa ubunifu. Jumba hilo linatoa jukwaa kwa wasanii wa Kitanzania, chipukizi na waliobobea, na linaendesha programu ya Rangi Nyumbani Residency inayowaunganisha wabunifu wa ndani na mitandao ya kimataifa.

Ushiriki wa Art OnO 2026 ni mara ya pili kwa jumba hilo kushiriki katika maonesho ya kimataifa, baada ya kushiriki kwa mara ya kwanza nchini Afrika Kusini mwaka 2025.Tanzania haijawahi kukosa vipaji vya sanaa. Kilichokosekana ni miundombinu, majukwaa na madaraja ya kuunganisha vipaji hivyo na dunia. Kupitia juhudi kama hizi, Rangi Gallery inaendelea kujenga madaraja hayo hatua kwa hatua, ikiipa sanaa ya Kitanzania nafasi yake stahiki katika jukwaa la kimataifa.
The post RANGI GALLERY YAREJEA KUTOKA SEOUL IKIWA IMEITANGAZA TANZANIA KIMATAIFA KUPITIA SANAA appeared first on SwahiliTimes.










Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!