KOCHA Mkuu wa Simba, Steve Barker, amesema kikosi chake kipo tayari kwa changamoto ya mashindano ya Kombe la Muungano, akisisitiza kuwa maandalizi yao yamekamilika na morali ya wachezaji iko juu kuelekea michuano hiyo.
Barker amesema baada ya mchezo wao wa hivi karibuni dhidi ya Namungo FC, waliwapa wachezaji mapumziko mafupi ya siku moja ili kurejesha nguvu kabla ya kuanza maandalizi rasmi ya michuano hiyo.
Ameeleza kuwa kwa sasa akili na nguvu za timu hiyo zimeelekezwa kikamilifu katika kuhakikisha wanapambana kutwaa taji la Kombe la Muungano.
Anaamini kikosi walichonacho kina uwezo wa kukidhi matarajio ya mashabiki wa klabu hiyo kubwa.
Kocha huyo ameongeza kuwa Simba ina kikosi imara chenye ushindani mkubwa ndani yake, hali inayowapa nafasi nzuri ya kufanya vyema katika kila mchezo watakaocheza.
“Tunakwenda na wachezaji wote ambao tumekuwa tukiwatumia, na tuna uhakika wa kuwa na nguvu ya kutosha. Kila mchezo tutaucheza kwa umakini mkubwa ili kuhakikisha tunafikia malengo yetu,” amesema Barker.
Amesisitiza kuwa lengo lao si tu kufika hatua za juu, bali ni kuhakikisha wanaingia fainali na hatimaye kunyanyua kombe hilo, jambo ambalo litakuwa faraja kwa mashabiki na uongozi wa klabu.
Kwa kauli hiyo, ni wazi kuwa Simba inaingia katika mashindano ya Kombe la Muungano ikiwa na dhamira ya dhati ya kufanya makubwa na kurejesha heshima yake kwa kutwaa ubingwa.
The post SIMBA YATINGA MUUNGANO KIVITA, BARKER ATOA SILAHA ZOTE appeared first on Soka La Bongo.











Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!