
Upelelezi wa kesi ya kutishia kuua na udhalilishaji inayowakabili wanafunzi watatu wa Vyuo Vikuu Dar es Salaam bado haujakamilika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Washtakiwa katika kesi hiyo ni Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Mary Matogolo (22), Ryner Mkwawili (22) Mwanafunzu wa Chuo Kikuu Ardhu na Asha Juma (22) wa Chuo Kikuu cha Uhasibu.
Kesi hiyo imetajwa leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Aaron Lyamuya ambapo Wakili wa Jamhuri, Erick Kamala amesema upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika, hivyo wanaomba ahirisho.
Baada ya kueleza hayo, Hakimu Lyamuya ameahirisha kesi hiyo hadi July 14, 2025 huku akisema dhamana inaendelea kwa washtakiwa hao.
Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka nane ikiwemo, kula njama ya kutenda kosa, kuchapisha taarifa za uongo kwa lengo la kumkashifu mtu anayeitwa Magnificant Kimario.
Kosa jingine ni kutishia kumuua Magnificant Kimario kwa kutumia kisu, kosa ambalo wanadaiwa kulitenda Machi 16, 2025 eneo la Sinza Dar es Salaam.
Hatua ya wanafunzi hao kufikishwa mahakamani, inakuja baada ya kusambaa kwa video yao ikionesha wakigombana na kumtaja mtu aliyefahamika kwa jina la Mwijaku ambapo baada ya kuhojiwa na Polisi walithibitisha mtu huyo ni Burton Mwemba ‘Mwijaku’.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!