
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amewataka vijana nchini kutumia mitandao ya kijamii kama fursa ya kujifunza na kujikwamua kiuchumi badala ya kuyatumia kwa matusi, upotoshaji na kuchochea chuki hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu.
Akizungumza Jumatano katika jengo la ofisi za wizara hiyo Mtumba, jijini Dodoma, Msigwa amesema serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu, hasa vijana, wanaotumia mitandao ya kijamii kwa njia zisizofaa.
Katika hotuba hiyo, Msigwa pia amegusia hali ya taharuki ya kisiasa inayoshuhudiwa katika vipindi vya uchaguzi, akibainisha kuwa baadhi ya wanasiasa hutumia vijana kama chombo cha kusambaza matusi, taarifa za upotoshaji na kushambulia watu mitandaoni.
Msigwa amesema hoja ya “sikujua” haiwezi kuwa sababu ya kutokuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria, na kwamba elimu ya matumizi sahihi ya mitandao imeshatolewa kwa kiwango kikubwa nchini.
“Wengi tunaowakamata wanasema ‘sikujua’. Lakini kutokujua sheria si kinga”, – amesisitiza.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!