Search
Sign In
2 Register
Your Cart 2 items
Subtotal : $1559

MYANMAR YAFANYA DURU YA MWISHO YA UCHAGUZI

  • 42
Scroll Down To Discover

Kiongozi wa serikali ya kijeshi ya Myanmar, Min Aung Hlaing, akipiga kura katika kituo cha kupigia kura cha Zayarthiri siku ya uchaguzi mkuu mjini Naypyitaw, MyanmarWatu wakiwa kwenye foleni kupiga kura katika kituo cha kupigia kura wakati wa uchaguzi mkuu wa Myanmar mjini Naypyitaw, Myanmar

Na. Meleka Kulwa- Fullshangwe Blog, Dodoma 

YANGON, Myanmar— Upigaji kura duru ya mwisho ulifanyika Jumapili , January 25,2026 nchini Myanmar katika uchaguzi mkuu wa awamu tatu, ukihitimisha mchakato uliodumu kwa takribani mwezi mmoja ambao tayari umeihakikishia serikali ya kijeshi na washirika wake wingi wa viti bungeni kwa ajili ya kuunda serikali mpya.

Wakosoaji wanasema uchaguzi huo haukuwa huru wala wa haki, na ulilenga kuhalalisha mamlaka ya jeshi baada ya kuiondoa madarakani serikali ya kiraia iliyochaguliwa ya Aung San Suu Kyi mnamo Februari 2021.

Chama kinachoungwa mkono na jeshi, Union Solidarity and Development Party (USDP), tayari kilishinda viti vingi vilivyoshindaniwa katika duru mbili za awali. Asilimia 25 ya viti katika mabunge ya juu na chini ya Bunge la Taifa vinahifadhiwa kwa ajili ya jeshi, hatua inayohakikisha jeshi na washirika wake kudhibiti Bunge.

Jenerali Mkuu Min Aung Hlaing, kiongozi wa serikali ya sasa ya kijeshi, anatarajiwa kwa kiasi kikubwa na wafuasi pamoja na wapinzani wake kuchukua nafasi ya Rais pindi Bunge jipya litakapokutana.

Upigaji kura waathiriwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe

Mapinduzi ya jeshi ya mwaka 2021 yalisababisha upinzani mkubwa ulioingiza Myanmar katika vita vya wenyewe kwa wenyewe. Sababu za kiusalama zilizotokana na mapigano zilisababisha upigaji kura kutofanyika katika zaidi ya theluthi moja ya manispaa 330 za nchi hiyo, jambo lililoongeza madai kuwa mchakato huo haukuwa huru wala wa haki.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Malaysia, Mohamad Hasan, alisema Jumanne kuwa Jumuiya ya ASEAN, ambayo Myanmar ni mwanachama, haikutuma waangalizi na haitathibitisha matokeo ya uchaguzi huo, akitaja ukosefu wa ushiriki wa wote na uhuru katika mchakato wa upigaji kura.

Akijibu ukosoaji huo, Min Aung Hlaing alisema kuwa, “Watu wanaoishi Myanmar ndio wanaopiga kura, si watu wa nje.”

Amebainisha kuwa, “Hatujali kama nchi za nje zitautambua uchaguzi huu au la. Tunatambua kura ya wananchi wetu.” Alisema hayo baada ya kukagua kituo cha kupigia kura mjini Mandalay, jiji la pili kwa ukubwa nchini humo.

Alipoulizwa kama atashiriki katika serikali mpya, alikataa kutoa maelezo, akisema Rais atachaguliwa Bunge litakapokutana.

Upinzani wakuu washiriki

Aung San Suu Kyi, aliyekuwa kiongozi wa Myanmar mwenye umri wa miaka 80, na chama chake hawakushiriki katika uchaguzi huo. Suu Kyi anahudumia kifungo cha miaka 27 jela kwa tuhuma zinazotajwa na wengi kuwa za kisiasa. Chama chake, National League for Democracy (NLD), kilishinda kwa kishindo uchaguzi wa mwaka 2015 na 2020, lakini kililazimishwa kuvunjwa mwaka 2023 baada ya kukataa kusajiliwa chini ya sheria mpya za kijeshi.

Vyama vingine pia vilikataa kusajiliwa au kushiriki kutokana na mazingira yasiyo ya haki, huku makundi ya upinzani yakihamasisha kususia uchaguzi.

Sheria mpya ya Ulinzi wa Uchaguzi imeweka adhabu kali kwa ukosoaji wa umma dhidi ya uchaguzi huo, na zaidi ya watu 400 wameripotiwa kushtakiwa hivi karibuni kwa makosa kama kusambaza vipeperushi au kuandika maoni mtandaoni.

Upigaji kura na matukio ya usalama

Upigaji kura ulianza saa 12:00 asubuhi na kumalizika saa 10:00 jioni katika manispaa 61 zilizopo katika mikoa sita na majimbo matatu, yakiwemo maeneo yaliyoshuhudia mapigano katika miezi ya karibuni.

Katika kituo cha kupigia kura eneo la Dagon, jijini Yangon, mzee mwenye umri wa miaka 86, Soe Tint, alisema alipiga kura kwa matumaini ya kuona nchi inapata amani na maendeleo katika sekta zote ikiwemo elimu.

Lakini mpiga kura mwingine, Lae Lae Yi (62), alisema hana matumaini makubwa.

“Sitarajii chochote, kwa sababu hakuna motisha,” alisema.

Mapigano yaliripotiwa kutokea katika angalau manispaa moja iliyofanya uchaguzi, na watu watano kujeruhiwa, kwa mujibu wa vyombo huru vya mtandaoni ikiwemo The Irrawaddy.

Maeneo mengi hayakupiga kura

Uchaguzi ulifanyika kwa awamu tatu kutokana na mapigano yanayoendelea. Duru mbili za awali zilifanyika Desemba 28 na Januari 11 katika manispaa 202 kati ya 330. Manispaa 67, nyingi zikiwa chini ya udhibiti wa makundi yenye silaha yanayopinga jeshi, hazikushiriki, hali iliyopunguza idadi ya viti vya Bunge kutoka 664 hadi 586.

Matokeo ya mwisho yanatarajiwa kutangazwa baadaye wiki hii. Serikali ya kijeshi imetangaza kuwa Bunge litakutana Machi, na serikali mpya kuanza kazi Aprili.

Chama kitakachopata wingi wa viti katika mabunge yote mawili kitachagua Rais, ambaye ataunda Baraza la Mawaziri na serikali mpya.

Zaidi ya wagombea 4,800 kutoka vyama 57 wanashindania nafasi za bunge la kitaifa na mabunge ya mikoa, ingawa ni vyama sita pekee vinavyoshindana kitaifa. Vyama 17 vingine vimepata viti vichache kuanzia kiti kimoja hadi 10.

Mwenyekiti wa People’s Party, Ko Ko Gyi, amesema mifumo ya uwajibikaji itadhoofika endapo chama kimoja kitapata udhibiti mkubwa wa Bunge.

Serikali ya kijeshi inasema kuna zaidi ya wapiga kura milioni 24, idadi ambayo ni chini kwa asilimia 35 ikilinganishwa na mwaka 2020. Ushiriki wa wapiga kura katika duru mbili za awali ulikuwa kati ya asilimia 50 hadi 60.

Chanzo: Associated Press (AP News), Januari 25, 2026.



Prev Post YANGA YAPANGA KUWASHTUA AL AHLY
Next Post Nafasi 15 za Ajira Serikalini
Related Posts
Comments 0

    Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!

Leave A Comment
or

For faster login or register use your social account.

Connect with Facebook