

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 17 Juni 2025, ametembelea majeruhi wa ajali ya gari waliolazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu, mkoani Simiyu.
Katika ziara hiyo ya kuonesha mshikamano na kuwafariji waliopatwa na janga hilo, Rais Samia ametoa pole kwa majeruhi na familia zao, sambamba na kuhimiza utoaji wa huduma bora na za haraka kwa wote walioumia.
Aidha, Rais Samia ameendeleza juhudi za kukuza uchumi wa viwanda nchini kwa kuzindua rasmi Kiwanda cha Kuchakata Pamba cha Biosustain Tanzania Limited, kilichopo Meatu. Kiwanda hicho kinatarajiwa kuongeza thamani ya zao la pamba, kutoa ajira kwa wananchi na kuinua kipato cha wakulima wa mkoa wa Simiyu na maeneo jirani.
Ziara hii ni sehemu ya msururu wa mikakati ya Rais Samia ya kuimarisha huduma za kijamii na maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi katika ngazi ya mikoa na wilaya.

PICHA NA IKULU
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!