
MAGAZETI ya Leo Jumatatu 16 June 2025
MAGAZETI ya Leo Jumatatu 16 June 2025
Jeshi la Polisi limelazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya waumini wa Kanisa lq Glory of Christ Tanzania Church, maarufu kama Kanisa la Ufufuo na Uzima waliojitokeza kufanya ibada kisha kuingia barabarani wakiwa na mabango yenye jumbe mbalimbali.
Waumini hao wamejitokeza lilipo kanisa hilo eneo la Ubungo Jumapili Juni 15, 2025 ambapo baada ya kushusha maombi, waliinua mabango yenye ujumbe unaoonyesha kupinga kuzuiwa kuabudu ndani ya kanisa hilo.
Polisi waliwatawanya waumini hao kwa kutumia mabomu ya machozi muda mfupi baada ya kuingia barabarani wakiwa wamenyanyua mabango hayo.
Hatua ya Polisi kuzuia waumini hao kufanya ibada katika eneo hilo inatokana na Juni 2, 2025, Msajili wa Jumuiya za Kiraia, Emmanuel Kihampa kutangaza kulifuta kanisa hilo kutokana na kukiuka Sheria ya Jumuiya Sura ya 337, kwa kile alichoeleza limekuwa linatoa mahubiri yenye mwelekeo wa kisiasa.
Tangu wakati huo, kanisa hilo limekuwa likilindwa na askari Polisi wenye silaha.
Hata hivyo, kadri siku zilivyokwenda, ulinzi ulipungua huku utepe uliowekwa kuzuia watu kuingia na kutoka uliendelea kusalia.
Aidha Kanisa hilo limefungua kesi mahakamani kupinga hatua hiyo na kesi inaendelea.
Jumamosi, Juni 14, 2025 kupitia mtandao wa kijamii wa Askofu Gwajima ambaye pia ni Mbunge wa Kawe (CCM) jijini Dar es Salaam, alitangaza uwepo wa kusanyiko akiandika: “Waebrania 10:25, wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.”
Hata hivyo, Askofu Gwajima tangu asubuhi hajaonekana kwenye eneo hilo licha ya waumini wake kuendelea kuwepo.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!