
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Rais Samia Suluhu Hassan amesema chama hicho kinakwenda pamoja na maendeleo ya teknolojia kadiri inavyokuwa, hivyo kimependekeza kufanyika kwa mikutano ya kimtandao.
Rais Samia amesema Katiba ya CCM inakipa chama fursa ya kutunga kanuni za mikutano hiyo, hivyo kwa kuwa baadhi ya mikutano imeshaanza kufanyika na kwamba mikutano hiyo haipo kwenye maelekezo ya Katiba chama kimeamua kuiingiza mikutano ya kimtandao kwenye kanuni zitakazojadiliwa leo na kupitishwa ili isikiuke katiba.
Akizungumza katika mkutano mkuu maalumu wa CCM Taifa leo Mei 29, 2025 Jijini Dodoma, Rais Samia amesema hilo ni pendekezo la kwanza ambalo wajumbe wa mkutano huo watatakiwa kulijadili.
“Chama chetu cha Mapinduzi kinaendelea jinsi dunia inavyoendelea, ndani ya chama chetu cha mapinduzi sasa tunafanya kazi kidigitali pia. Tumefunga mitambo ya kuweza kuwasiliana na mikoa na wilaya ili kurahisisha utendaji wa kazi,”
“Tumekuja na wazo la E-meetings (Mikutano ya kimtandao) ambayo Idara ya Oganaizesheni inapendekeza vikao vifuatavyo vifanyike kwa njia ya mtandao…Kikao cha kwanza ni Sekretarieti ya Wilaya, kamati ya siasa ya wilaya, Sekretarieti ya mkoa, Kamati ya siasa ya mkoa, Sekretarieti ya kamati maalumu ya halmashauri kuu ya CCM Taifa, Sekretarieti ya Halmashauri kuu ya CCM Taifa, Kamati Maalumu ya Halmashauri kuu ya CCM Taifa, Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM, Halmashauri kuu ya CCM Taifa na Mkutano Mkuu wa Taifa.” amesema Rais Samia
Ameongeza kuwa mikutano hiyo itafanyika kwa njia ya mtandao endapo tu kutakuwa na ulazima na kwamba ile ya ngazi ya wilaya na mkoa itafanyika kwa idhini ya Katibu Mkuu wa CCM Taifa.
Rais Samia ameelekeza hilo lifanyike ili kuepusha kutumika vibaya kwa mitandao kupitia vikao hivyo.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!