
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imetoa tahadhari kwa Watanzania wanaoishi au wanaopanga kusafiri kwenda katika nchi za Mashariki ya Kati, zikiwemo Bahrain, Israel, Kuwait, Qatar, Falme za Kiarabu (UAE) na Oman.
Katika taarifa, Serikali imewahimiza raia wote kuchukua tahadhari stahiki katika nyakati hizi na kufuata maelekezo ya mamlaka husika za nchi wanazoishi au wanazokusudia kusafiri.
Watanzania waliopo katika eneo hilo la Mashariki ya Kati wameshauriwa kuepuka kufanya safari za kuingia au kutoka kwa sasa, badala yake kubaki katika makazi yao inapowezekana, kufuata maagizo ya mamlaka za usalama, na kuepuka maeneo yenye shughuli za kijeshi au kiusalama.
Aidha, wametakiwa kutumia njia rasmi za mawasiliano, pamoja na kuhifadhi pasipoti na vitambulisho vya Tanzania katika maeneo salama na yanayopatikana haraka endapo kutatokea dharura.
Serikali pia imewasihi Watanzania walioko Mashariki ya Kati kujisitiri kwa uangalifu na kuendelea kufuatilia mawasiliano rasmi kutoka kwa balozi na njia za dharura. Kwa ajili ya ufuatiliaji wa karibu, Watanzania wametakiwa kujisajili kupitia kiunganishi rasmi cha Wizara ya Mambo ya Nje.

The post Serikali Yatoa Tahadhari kwa Watanzania Walioko Mashariki ya Kati appeared first on Global Publishers.






Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!