KIKOSI cha Simba SC leo kinatupa karata yake ya kwanza katika michuano ya Kombe la Shirikisho la CRDB kwa kuvaana na Greenland, katika mchezo utakaopigwa saa 1:00 usiku kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo.
Simba inaingia dimbani ikiwa na morali kubwa baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Stade Malien kwenye mchezo wao wa mwisho wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Ushindi huo umeongeza hali ya kujiamini kwa wachezaji na benchi la ufundi, wakiamini wanaweza kuendeleza matokeo mazuri katika mashindano ya ndani.
Katika mchezo huo wa kimataifa, Simba ilionyesha muunganiko mzuri wa kikosi pamoja na ari ya hali ya juu ya kupambana hadi dakika za mwisho.
Benchi la ufundi limeeleza kuwa litaendelea kuboresha makosa madogo yaliyojitokeza ili kuhakikisha timu inakuwa imara zaidi inapowania taji la Kombe la Shirikisho.
Kocha Mkuu wa Simba, Steven Barker, amesema mchezo wa leo ni muhimu kwao kuanza kwa ushindi na kuweka msingi mzuri wa safari ya ubingwa.
“Ni mashindano muhimu kwetu. Tunahitaji kuanza kwa nguvu na kupata ushindi ili kuweka mazingira mazuri ya kutwaa taji. Wachezaji wako kwenye hali nzuri na wameonesha kiwango bora katika mchezo uliopita,” amesema Barker.
Mbali na pambano hilo, ratiba ya Kombe la Shirikisho la CRDB leo pia itashuhudia KMC FC ikichuana na Bandari FC katika mechi inayotarajiwa kuwa na ushindani mkali, huku kila upande ukisaka ushindi wa kusonga mbele kwenye michuano hiyo.
The post SIMBA SAFARI YA UBINGWA MEJA JENERALI ISAMUHYO appeared first on Soka La Bongo.






Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!