OFISA Habari wa Yanga SC, Ali Kamwe, amesema hasira za kuondolewa katika hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika wamezihifadhi kifuani, wakisubiri kuzimalizia kwenye mchezo ujao wa Kariakoo Derby dhidi ya watani wao wa jadi.
Kamwe amesema wanafahamu wazi kuwa kuondolewa kwao kumewapa furaha wapinzani wao, lakini wanaamini furaha hiyo haitadumu kwani watakutana nao uwanjani katika Ligi Kuu Tanzania Bara.
Ameongeza kuwa kikosi hicho kimehamishia nguvu zote kwenye maandalizi ya dabi hiyo, wakilenga kuonyesha majibu kupitia matokeo.
Yanga watakuwa wenyeji katika mchezo huo utakaopigwa Machi Mosi kwenye dimba la New Amaan Complex visiwani Zanzibar, huku Simba SC wakiingia uwanjani kama wageni. Mchezo huo unasubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka nchini kutokana na ushindani wa jadi uliopo kati ya timu hizo mbili.
Klabu ya Yanga ilitupwa nje ya mashindano ya CAF Champions League msimu wa 2025/26, ikiishia katika hatua ya makundi licha ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya JS Kabylie katika mechi iliyochezwa Februari 15, 2026, Zanzibar. Ushindi huo haukutosha kuwavusha kwenda robo fainali kutokana na matokeo ya mechi nyingine katika kundi lao.
Akizungumzia hali hiyo, Kamwe amesema matokeo hayo yanaumiza, lakini yamewapa somo muhimu la kuhakikisha msimu ujao hawafiki hatua ya kusubiri matokeo ya mechi nyingine ili kujua hatima yao.
“Tunasahau matokeo yaliyopita sasa tunarejea kujiandaa na Ligi Kuu, Niwakumbushe wale wanaotucheka, hasira zetu zipo kifuani. Tukutane Machi Mosi, New Amaan Complex, tutamaliza hasira zetu dhidi ya mtani wetu,” amesema Kamwe.
The post BAADA YA KUAGA CAF, YANGA WAITAZAMA SIMBA appeared first on Soka La Bongo.











Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!