

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limewataka waumini wa Kanisa la Deliver Hope for All Nations lililopo Kata ya Kizumbi, Wilaya ya Shinyanga, kutojisumbua kusikiliza maneno ya mitandaoni yenye lengo la kuvuruga amani.
Akitoa elimu kuhusu amani Oktoba 26, 2025, Polisi Kata ya Kizumbi, Mkaguzi wa Polisi Yefta Kwelebela, alisema ni muhimu wananchi kujiepusha na taarifa za upotoshaji zinazotolewa mitandaoni ambazo zinaweza kuhatarisha amani ya nchi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Shinyanga, Mkaguzi wa Polisi Jane Mwazembe, alitoa elimu kuhusu ukatili wa kijinsia na kazi za Dawati hilo ni kitengo maalum ndani ya Jeshi la Polisi kinachoshughulikia makosa ya ukatili kama vile kubaka, kulawiti, mimba za utotoni, ndoa za utotoni, na kutelekeza familia. Alisisitiza kuwa wahanga wakubwa wa ukatili ni watoto na wanawake, lakini Dawati hilo linawahudumia pia wanaume ingawa ni wachache wanaojitokeza kuripoti.

Kwa upande wake, Askofu Mkuu wa Kanisa hilo, Kuhani Ayubu Mwakibinga, aliwataka waumini wake kujitokeza Oktoba 29, 2025, kutimiza haki zao za kikatiba kwa kupiga kura kwa amani.
“Taifa letu la Tanzania limejengwa kwa misingi ya Sheria na Katiba, hivyo basi tumieni haki yenu ya kikatiba kwa kupiga kura kwa amani, kwa sababu ni haki yenu” alisema Askofu Mwakibinga.












Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!