KUELEKEA mchezo wa Kariakoo Derby utakaopigwa kesho, Kocha Mkuu wa Yanga SC, Pedro Gonçalves, ameweka wazi kuwa hali ya kiungo mshambuliaji Pacome Zouzoua bado haijawa ya uhakika, jambo linaloibua maswali mengi kuelekea pambano hilo kubwa.
Yanga inatarajiwa kushuka kwenye dimba la New Amaan Complex visiwani Zanzibar kuwakaribisha watani zao, Simba SC, katika mchezo utakaopigwa saa 2:15 usiku, ukiwa umebeba presha na matarajio makubwa kwa pande zote mbili.
Akizungumza kuelekea dabi hiyo inayosubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka nchini, Gonçalves amesema benchi la ufundi bado halijafanya maamuzi ya mwisho kuhusu uwepo wa nyota huyo kikosini.
Amesisitiza kuwa licha ya Zouzoua kuonyesha dalili nzuri za kuimarika, bado wanahitaji kujiridhisha kikamilifu na utimamu wake kabla ya kumpa jukumu katika mechi yenye ushindani mkubwa kama huo.
“Mazoezi ya mwisho ya leo Jumamosi yatakuwa na uzito mkubwa katika kuamua hatma ya mchezaji huyo. Tutapima uwezo wake wa kumudu kasi na presha ya dabi kabla ya kufanya uamuzi wa mwisho kama ataanza, atakuwa benchi au hatakuwepo kabisa kwenye kikosi cha siku ya mechi,” amesema Pedro.
Kauli hiyo imezua mjadala miongoni mwa mashabiki wa Yanga, wengi wakitambua umuhimu wa Zouzoua katika safu ya ushambuliaji.
Uwepo wake huongeza ubunifu, kasi na uwezo wa kutengeneza nafasi za mabao, hivyo kukosekana kwake kunaweza kuathiri mipango ya kiufundi ya timu hiyo.
Gonçalves ameonyesha kujiamini na kikosi chake, akisisitiza kuwa ana wachezaji wa kutosha wenye uwezo wa kuziba pengo lolote litakalojitokeza.
Kauli yake pia inatazamwa kama sehemu ya mbinu za kisaikolojia kuelekea dabi hiyo, huku Simba wakilazimika kusubiri hadi dakika za mwisho kujua hatma halisi ya kiungo huyo hatari.
The post SIMBA KAA TAYARI, PEDRO AFICHA KADI YAKE KUTUFU appeared first on Soka La Bongo.






Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!