OFISA Habari wa klabu ya Yanga , Ali Kamwe, amesema kikosi chao kinatambua ugumu wa mchezo wa leo dhidi ya Namungo FC, akisisitiza kuwa kuwafunga wapinzani hao wa Ruangwa si jambo rahisi, hata kuliko kuifunga Simba SC.
Yanga wanashuka dimbani leo katika Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Lindi, wakiwa na lengo la kuvuna alama tatu muhimu ili kuendelea kujiimarisha kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Namungo wakiwa nyumbani, wanatarajiwa kutoa upinzani mkali mbele ya mashabiki wao katika mchezo huo.
Akizungumza kuelekea mchezo huo, Kamwe amesema kikosi kimewasili salama mkoani Lindi na maandalizi yamekamilika kwa asilimia kubwa, wachezaji wakiwa na morali ya juu kupambana kuhakikisha wanapata ushindi.
“Huu ni mchezo mgumu na wa ushindani mkubwa kwa sababu tunacheza ugenini dhidi ya timu ambayo imejipanga vizuri. Tumekuja kupambana kusaka alama muhimu. Kwetu sisi, wakati mwingine kumfunga Simba ni rahisi kuliko kuifunga Namungo FC,” amesema Kamwe.
Kauli hiyo inaonyesha namna Yanga wanavyochukulia kwa uzito mchezo huo, wakitambua kuwa Namungo imekuwa ikipeleka upinzani mkali kila wanapokutana, hasa wanapocheza katika dimba lao la nyumbani.
The post LEO HATUTANII, NAMUNGO WAGUMU KULIKO SIMBA, KAMWE appeared first on Soka La Bongo.






Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!