MWENYEKITI klabu ya Simba, Murtaza Mangungu, amesema timu yake inarejea nyumbani ikiwa na matumaini makubwa ya kulipiza kisasi dhidi ya Al Masry katika mchezo wa marudiano wa Kombe la Shirikisho Afrika utakaofanyika kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Simba ilipoteza mchezo wa kwanza kwa mabao 2-0 dhidi ya Al Masry katika uwanja wa Suez, Misri. Hata hivyo, Mangungu amesisitiza kuwa wachezaji wake wamemaliza dakika 90 za kwanza bila majeraha na sasa wanajiandaa kikamilifu kwa mchezo wa marudiano.
“Tulitengeneza nafasi nyingi lakini bahati haikuwa upande wetu. Tuna uwezo wa kuwafunga nyumbani, hivyo tunawasubiri kwa hamu Uwanja wa Benjamin Mkapa,” alisema Mangungu.
Aliwataka mashabiki wa Simba kuungana na timu yao kwa kuipa sapoti kubwa kuelekea mchezo huo muhimu.
Alisisitiza kuwa historia inawapa matumaini, akirejea kumbukumbu ya mechi dhidi ya Kaizer Chiefs ambapo Simba ilifungwa mabao 4-0 ugenini lakini ilijibu kwa ushindi wa mabao 3-0 nyumbani.
“Maandalizi ya mchezo wa marudiano yameanza rasmi. Tunataka kuonyesha uwezo wetu na kuhakikisha tunavuka hatua hii,” aliongeza Mangungu.
Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo, Simba inajipanga kutoa mapokezi mazuri kwa Al Masry kama walivyopokelewa Misri, huku akisisitiza kuwa kila Mwanasimba ana jukumu la kusaidia timu kushinda na kusonga mbele katika michuano hiyo.
The post KISA KIPIGO CHA JANA MISRI….SIMBA KUJA NA MBINU HII MPYA KWA MKAPA…. appeared first on Soka La Bongo.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!