

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Heche amesema hawakubaliani na maamuzi ya Msajili wa vyama wa kuwachagulia viongozi wao kinyume na Katiba yao na kuhusu kuzuia ruzuku ya chama hicho, hivyo watalipeleka suala hilo mahakamani.
Heche ameyasema hayo leo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema: “Kuhusu taarifa aliyoitoa Msajili wa Vyama vya Siasa ya kuzuia ruzuku ya chama (CHADEMA), tunaenda Mahakamani kwa sababu Msajili wa Vyama vya Siasa amechukua jukumu la kuzuia ruzuku ya chama chetu, sasa sheria anayoisimamia Msajili mwenyewe yaani Sheria ya Vyama Siasa, kifungu cha 18(6) kinasema Msajili ana uwezo wa kuzuia ruzuku ya chama kingine chochote cha siasa kinachopokea ruzuku pale tu ambapo kuna kweli ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa chama hicho”
“Kwamba labda chama kimefanya matumizi ya hovyo ya fedha na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) amekagua na ametoa ripoti, kama vile mnavyosikia ripoti ya CAG inasema serikali imefanya matumizi yasiyokuwa na tija, sasa kwetu sisi (CHADEMA) kama mkaguzi angekuwa amekagua tukapata hati chafu kwa mfano au fedha zimetumika vibaya, au jambo lingine lolote linalofanania na hilo, kwa mujibu wa kifungu hicho cha 18(6) hapo tu ndipo Msajili anapopata mamlaka ya kuzuia ruzuku” amesema Heche
Akaongeza: “Utaratibu wa jambo hili unaenda mpaka kwenye utaratibu ikiwemo barua, na hilo linaenda mpaka kwenye Baraza la Wadhamini la chama, kwa sababu chama hiki ni mali ya Baraza la Wadhamini, sasa ili hatua hiyo ifikiwe ni lazima chama kishindwe na Bodi ishindwe, na ripoti maalum za ukaguzi zioneshe kwamba kuna matumizi ya hovyo, sasa tunaenda Mahakamani kuonesha kutokubaliana na jambo hilo, tutawaelekeza wanasheria wetu ikifika Alhamisi, jambo liwe limeenda mahakamani.”
Na Elvan Stambuli GPL.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!