

Pwani, 24 Juni 2024: Katika jitihada za kukabiliana na changamoto ya ajali za barabarani, Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kupitia Kituo cha Umahiri wa Usalama Barabarani kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi, Kitengo cha Usalama Barabarani, wametoa elimu ya usalama barabarani kwa madereva wa malori, daladala, maafisa usafirishaji (Bodaboda) katika Wilaya ya Kibaha, Mkoani Pwani. Huku wakihimiza kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani ili kulinda maisha yao pamoja na abiria.

Akizungumza leo Juni 24, 2025 Wilayani Kibaha Mkoa Pwani, Mkuu wa Kituo cha Kikanda cha Umahiri katika Usalama Barabarani kutoka NIT, Bw. Godlisten Msumanje, amesema kuwa madereva wote wanapaswa kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani.
Amesisitiza umuhimu wa madereva wa bodaboda kuvaa kofia ngumu pamoja na kuepuka kubeba abiria zaidi ya mmoja ili kupunguza hatari ya ajali.

Bw. Msumanje ameongeza kuwa lengo la elimu hiyo ni kuwakumbusha madereva kuheshimu sheria na kutumia mbinu za udereva wa kujilinda ili kuepusha ajali zinazoweza kuzuilika.
Kwa upande wake, Mkaguzi wa Jeshi la Polisi kutoka Kikosi cha Usalama Barabarani Makao Makuu, Bi. Happyness Mndeme, amesema kuwa Jeshi la Polisi limejipanga kuhakikisha madereva wote wanapata elimu ya usalama barabarani kwa kutumia mbinu rafiki na zenye ufanisi.

Naye Mkaguzi wa Jeshi la Polisi Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani, Bw. Abas Mzambwa, amekipongeza Chuo cha NIT kwa kutoa elimu hiyo, huku akibainisha kuwa ni hatua muhimu hususan kwa madereva wa badaboda ambao mara nyingi huwa waathirika wakuu wa ajali.

Nao, Madereva waliopatiwa elimu hiyo, wakiwemo Daudi Masalu na Twaha Swalehe, wameishukuru NIT kwa elimu waliyopata, huku wakieleza kuwa elimu hiyo itakuwa msaada mkubwa katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa usalama zaidi.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!