
Cairo, Misri – Mshambuliaji wa Kimataifa kutoka DR Congo, Fiston Kalala Mayele, ameendelea kuthibitisha kuwa yeye ni miongoni mwa wakali barani Afrika baada ya kufunga bao muhimu katika ushindi wa Pyramids FC wa mabao 2-1 dhidi ya Mamelodi Sundowns katika fainali ya pili ya TotalEnergies CAF Champions League iliyopigwa kwenye Uwanja wa 30 June Air Defence Stadium jijini Cairo.
Baada ya sare ya 1-1 jijini Pretoria kwenye mchezo wa kwanza, ushindi huu uliipa Pyramids ushindi wa jumla wa mabao 3-2, na kuwa klabu ya nne kutoka Misri kutwaa taji hili la heshima kubwa barani Afrika, wakiungana na Al Ahly, Zamalek na Ismaily – jambo ambalo halijafikiwa na taifa lingine lolote.
Katika dakika ya 23, Mayele alifungua ukurasa wa mabao kwa shuti la chini lililoenda moja kwa moja kwenye kona ya mbali, baada ya kupokea pasi murua kutoka upande wa kulia. Hilo lilikuwa bao lake la tisa kwenye mashindano haya, likiongeza uzito wake kama mhimili wa mafanikio ya kihistoria ya Pyramids msimu huu.
Safari ya Mayele ni ya kishujaa. Akiwa ameibuka kuwa nyota akiwa na Yanga SC ya Tanzania, alisaidia klabu hiyo kutwaa mataji ya Ligi Kuu Tanzania Bara mfululizo na kufika fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF mwaka 2023 – mafanikio ambayo yaliweka jina lake kwenye ramani ya soka Afrika.
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!