

Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) limelaani shambulio la Marekani dhidi ya vituo vya nyuklia vya amani vya Iran katika taarifa yake ya jana (siku ya Jumapili), na kusisitiza kwamba wale wanaoishambulia Iran wanapaswa kutarajia jibu ambalo litawafanya wajute.
Taarifa ya jeshi la SEPAH imesema: “Asubuhi ya leo (jana), utawala wa kihalifu wa Marekani, kwa uratibu kamili na utawala wa Kizayuni, ulifanya jinai ya wazi na isiyo na kifani kwa kufanya mashambulizi haramu ya kijeshi dhidi ya vituo vya amani vya nyuklia vya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Hatua hii inakiuka wazi Mkataba wa Umoja wa Mataifa, sheria za kimataifa, Mkataba wa Kuzuia Uenezaji wa Nyuklia, na kanuni za msingi za kuheshimu uhuru, ardhi na mamlaka ya mataifa.”

Taarifa hiyo imeongeza kuwa: “Tangu dakika za mwanzo za uchokozi wa Wazayuni, ilidhihirika wazi kwa jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwamba, kuna uungaji mkono na usaidizi kamili wa Marekani katika kupanga na kutekeleza uchokozi huu.”
Sehemu nyingine ya taarifa ya Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu SEPAH imesema: “Kukariri Marekani makosa yake ya hapo awali yaliyoshindwa kunaonyesha uzembe wake wa kimkakati na kutozingatia hali halisi katika eneo. Badala ya kujifunza kutokana na kushindwa kwake mara kwa mara, Washington imeanzisha mashambulizi ya moja kwa moja kwenye vituo vya amani vya nyuklia, ikijiweka kwenye mstari wa mbele wa uchokozi huu.”
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!