

Dar es Salaam, 10 Juni 2025: Hatua madhubuti za mageuzi zilizoasisiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan, zimeanza kuzaa matunda makubwa baada ya Serikali kupokea gawio na michango mingine ya kihistoria ya Sh1.028 trilioni kutoka kwa mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali ina hisa.

Takwimu hizi ni matokeo ya utekelezaji wa mikakati ya kuongeza tija na ufanisi katika utendaji wa taasisi, ikiwa ni muendelezo wa maelekezo ya Rais Samia kuhusu uwajibikaji na ufanisi wa taasisi za umma tangu alipoingia madarakani.
Akizungumza katika tukio hilo maalumu la “Gawio Day”, Rais Samia alisema kuwa makusanyo hayo ni ishara ya mabadiliko ya kiutendaji yanayolenga kujenga taasisi imara, zenye uwezo wa kujitegemea na kuchangia kikamilifu maendeleo ya Taifa.

“Nimefurahishwa sana na ongezeko hili la mapato lisilo na mfano tangu kuanzishwa kwa Ofisi ya Msajili wa Hazina mwaka 1959. Hii ni hatua kubwa katika safari yetu ya mageuzi,” alisema Rais Samia.
Ameongeza kuwa pamoja na mafanikio hayo, bado Serikali ina malengo makubwa zaidi — ikiwemo kuvuka kiwango cha Sh1.5 trilioni kwa mwaka ujao — ikiwa ni sehemu ya dira ya kujenga mashirika yenye ufanisi mkubwa, yanayochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Kwa mujibu wa Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, mafanikio haya yametokana na ufuatiliaji makini, usimamizi thabiti, pamoja na utekelezaji wa falsafa ya Rais ya “R4”, hususan kipengele cha “Reforms and Rebuild”.
Katika msisitizo wa mageuzi zaidi, Mhe. Rais ametoa maagizo manne muhimu kwa taasisi ikiwemo: ubunifu katika kutatua changamoto na kuongeza tija, kukamilisha sheria ya uwekezaji wa Umma, kuimarisha mifumo ya TEHAMA kwa ufanisi zaidi, na kuwajengea watumishi uwezo na kutoa motisha stahiki.
“Tusisubiri kila tatizo kutatuliwa na Serikali. Tuwe wabunifu, tutumie fursa kama soko la mitaji kuboresha utendaji wetu,” alisema Rais Samia huku akiwataka viongozi wote wa taasisi kushiriki kikamilifu katika safari ya mageuzi.
Kampuni ya Puma Energy Tanzania haikubaki nyuma katika mchakato huu kwani ilichangia kiasi cha shilingi bilioni 13 kama gawio. Akizungumza mara baada ya hafla hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Bi. Fatma Abdalla alisema, “Tunajivunia kuwa sehemu ya tukio hili la kihistoria kwa taifa. Mchango wetu unaakisi uwazi, ubora wa utendaji, na dhamira ya Puma Energy Tanzania katika kuiunga mkono Tanzania yenye ajenda ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.”
Katika mwaka wa fedha 2024/25, taasisi 213 zimechangia Sh1.028 trilioni, sawa na ongezeko la asilimia 68 ukilinganisha na mwaka jana. Hii ni sehemu ya mafanikio yanayoimarisha msingi wa uchumi wa nchi kupitia mashirika binafsi
ReplyForward |
Hakuna maoni bado. Kuwa wa kwanza kuandika maoni!